Waziri wa Fedha, Mhe. Dkt. Mwigulu Lameck Nchemba (Mb), amekutana na kufanya mazungumzo na Ujumbe wa Benki ya Maendeleo ya Italia (CDP International Development Cooperation), ukiongozwa na Mkurugenzi Mtendaji wa Benki hiyo, Bw. Dario Scannapieco, Mjini Rome Italia, ambapo pamoja na mambo mengine, walijadiliana kuhusu namna Tanzania na Benki hiyo, zitakavyoshirikiana katika utekelezaji wa miradi ya kiuchumi na kijamii ikiwemo kilimo (usalama wa chakula), kukuza uzalishaji viwandani, usalama wa nishati na miundombinu endelevu, sekta ya maji, afya, elimu na mafunzo pamoja na kuiwezesha sekta binafsi kushiriki katika shughuli za kukuza uchumi wa nchi.
Miongoni mwa maeneo ambayo Taasisi hiyo inaisaidia Tanzania ni pamoja na sekta ya elimu ambapo imetoa ufadhili wa ujenzi wa vyuo vya ufundi vya elimu ya juu ikiwemo Karume Institute of Science and Technology, Arusha Technical College, Mbeya University of Science and Technology na Dar es Salaam Institute of Technology, ambavyo vinatarajia kutoa usaidizi wa kukuza ujuzi na ajira hususan kwa vijana.